Tiba Za Kisukari: Chakula Na Mazoezi Kwa Mgonjwa Wa Kisukari

 

Hapo zamani, kabla ya uvumbuzi wa insulin (1921), ugonjwa wa kisukari, Type 1 Diabetes, ulikuwa ni ugonjwa ulioua watu wengi sana miaka michache tu baada ya mtu kuupata ugonjwa huo. Lakini sasa mambo yamebadilika kwa kiasi kikubwa sana. Mtu mwenye ugonjwa huu anaweza kuishi maisha ya kawaida kabisa, ili mradi anakuwa na mpango mzuri wa chakula, mazoezi ya kutosha na anatumia insulin. Kuwa mgonjwa wa kisukari maaana yake ni kukubali namna ya kuishi na siyo kushindwa kufanya jambo lo lote lile ulilokusudia. Unaweza kufanya biashara zako, kushiriki michezo na kufikia malengo yako bila tatizo lo lote.

Kuna orodha ya watu wengi waliokutwa na kisukari na wakafanya vizuri katika michezo, siasa, uigizaji wa filamu, muziki, uandishi wa habari n.k. Kinachotakiwa ni kuwa na mpango mzuri wa kula, mazoezi ya kutosha na kuzingatia tiba unayopewa na daktari wako. Hakuna sababu KAMWE ya kushindwa kufikia malengo yako. Mfano mzuri ni Sir Steven Redgrave, mwanamichezo aliyeweza kunyakua medali za dhahabu katika michezo ya Olympiki kwa miaka mitano mfululizo akiwa mwathirika wa Type 1 Diabetes kuanzia mwaka 1997.

Mgonjwa wa kisukari anapaswa kuchukua vipimo mara kwa mara ili kujua kiwango cha sukari alicho nacho, anapaswa vilevile kuhakikisha kuwa anapima blood pressure na kudhibiti kiwango cha cholesterol kwani vinaweza kumsababishia magonjwa ya moyo.

Kisukari Cha Juu Na Kisukari Cha Chini

Mgonjwa anatakiwa ahakikishe kiwango chake cha sukari katika damu hakibadiliki sana. Kuwa na kiwango kidogo cha sukari katika damu (Hypoglycemia) kuna madhara mengi katika mwili wa mgonjwa kama vile ilivyo kwa mgonjwa kuwa na kiwango kikubwa cha sukari katika damu (Hyperglycemia).

 

Mpango Wa Chakula Kwa Mgonjwa Wa Kisukari

 

Mgonjwa wa kisukari hana masharti ya ajabu kuhusu chakula anachotakiwa kula, kimsingi anaweza kula chakula cho chote anachopenda. Kuna mambo matatu ambayo yanabidi kuangaliwa katika kuweka kiwango cha sukari cha mgonjwa kwenye kiwango kinachofaa. Mambo hayo ni:

  • Ni chakula gani
  • Chakula hicho kinaliwa kwa kiasi gani
  • Chakula hicho kinaliwa muda gani

Watalaamu wa afya na mambo ya chakula wanabainisha kwamba chakula kinachotakiwa kuliwa kwa wingi zaidi ni chakula chenye wanga (carbohydrates), kikifuatiwa na mboga na matunda, kisha chakula chenye protini na mwisho ni chakula chenye mafuta (fats). Wataalamu na washauri wa magonjwa ya kisukari wanamshauri mgonjwa wa kisukari kupata chakula kwa mpango huo huo.

Chakula Chenye Wanga

Chakula chenye wanga hupatikana zaidi kutoka kwenye nafaka, mboga, maziwa ya mgando na matunda.

Mwili wa binadamu huhitaji chakula chenye wanga, hatuwezi kuishi bila chakula cha aina hii. Mwili hubadilisha wanga na kuwa glucose-aina ya sukari ambayo hutumiwa na seli za mwili kwa ajili ya kupata nguvu na kukua.

Imeonekana kuwa mtu akila kiasi kile kile cha chakula chenye wanga na muda ule ule kila siku, anakuwa na nafasi kubwa sana ya kudhibiti kiwango chake cha sukari katika mwili. Ni muhimu kuhakikisha kuwa mgonjwa haruki mlo wo wote kwani kufanya hivyo kutasababisha badiliko kubwa la kiwango cha sukari katika damu yake kitu ambacho kinatakiwa kikwepwe kwa mgonjwa wa kisukari. Kuwa na ongezeko la glucose katika damu ambalo ni la kawaida kunasaidia kuweza kujua namna ya kuweka uwiano kati ya chakula, dawa na mazaoezi ya mwili na hivyo kudhibiti kiwango cha sukari katika mwili wa mgonjwa.

Uwiano mzuri wa chakula chenye wanga, protini na mafuta umeonekana kuwa:

  • Wanga asilimia 45-65
  • Protini asilimia 15-20
  • Mafuta asilimia 20-35

Kuchanganya aina tofauti tofauti za nafaka, matunda na mboga kumeonyesha kusaidia zaidi na mboga zinasidia kupunguza sukari mwilini kwa sababu ya nyuzinyuzi zake. Hilo pia ni sahihi kwa nafaka ambazo ni nzima, zile ambazo hazikukobolewa.

 

Mazoezi Ya Mwili Kwa Mgonjwa Wa Kisukari

 

Mazoezi ya mwili kwa mtu anayeishi na tatizo la kisukari ni muhimu kwa sababu zifuatazo:

  • yanasaidia katika kudhibiti kiwango cha sukari katika mwili
  • yanasaidia kupunguza uzito wa mwili
  • yanasaidia kudhibiti blood pressure
  • yanasaidia kuweka cholesterol kwenye kiwango kizuri

 

 

mazoezi kwa mtu wa kisukari

 

Pamaoja na faida hizi hapo juu, mazoezi pia yanasaidia kupata usingizi mzuri na kupunguza msongo wa mawazo. Inashauriwa kufanya mazoezi angalau kwa siku tano katika wiki na mazoezi hayo yawe ya kawaida, siyo ya nguvu, ambayo yatafanywa kwa muda usiopungua nusu saa kila siku. Mazoezi ambayo unaweza kuyafanya ni pamoja na kutembea kwa mwendo wa haraka, kuogelea, kuendesha baiskeli kwenye sehemu ya tambalale au milima ya kadri, kucheza muziki au hata kukata majani kwenye bustani.

Kama hujafanya mazoezi kwa muda mrefu, anza na mazoezi madogo na kuongeza viwango taratibu. Zingatia kuwa mazoezi yawe kama ya nusu saa kila siku na yafanywe angalau kwa siku tano katika wiki na siyo mazoezi ya saa mbili mara moja kwa wiki.

Unaweza kujiunga na gymn, sehemu ambayo utapata mtaalamu wa kutoa mazoezi kwa watu wenye matatizo mbalimbali. Kupata mtu wa kukusaidia na kukuelekeza katika mazoezi kutakupa ari ya kufanya mazoezi kwa umakini zaidi. Isitoshe, gymn zina vifaa vya kisasa vya kukupa vipimo vya mazoezi yako na maendeleo yako.

Katika ukurasa mwingine tutaona tiba ya kisukari kwa kutumia insulin.

Tafadhali usisite kuuliza maswali au kutoa maoni yako kuhusu mada yetu ya leo, tatafurahi sana kuona kuwa tumekujibu vizuri na kwa wakati.

Ukurasa  1    2    3   4

Pata Mahitaji Yako Ya Dawa Za Nje Kwa Matatizo Yanayokusumbua Ukiwa Tanzania. Boresha Afya Yako Kupitia Tovuti Hii